TANGAZA NASI KWA BEI NAFUU

Jumatano, 22 Mei 2013

MTWARA KIMENUKA TENA, MMOJA APOTEZA MAISHA


Pichani ni moja ya mitaa ya Mtwara iliyoathirka na vurugu za leo, kwa kuchomwa matairi Barabarani, na kuharibu nyumba za wananchi na Ofisi za Serikali.
*******************************************
Na Mwandishi Wetu, Mtwara
MTU mmoja amepoteza maisha, Wanne kujeruhiwa na 21 kutiwa mbaroni kufuatia vurugu zilizotokea leo Mkoani Mtwara baada ya Wananchi wa Mkoa huo kufunga baadhi ya mitaa na kuchoma matairi katika Barabara ya Zambia huku wakiharibu mali za wananchi na kuchoma Ofisi za Serikali pamoja na Nyumba ya Mwandishi wa Habari wa TBC.
Wananchi hao walianza kufanya vurugu hizo mara tu baada ya kusomwa kwa Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini Bungeni mjini Dodoma leo, ambapo walikuwa wakipinga kile kilichoelezwa kutengwa kwa Bajeti ya Ujenzi wa Bomba la kusafirishia Gesi kutoka mkoani humo hadi Jijini Dar es Salaam.
Wananchi hao walianza vurugu hizo kwa kuvunja Daraja la Mikindani ambalo ni muhimu kwa mawasiliano kutoka Lindi na Dar kuingia Mtwara. 
 Aidha Imeelezwa kuwa katika harakati za kuongeza nguvu ya askari wa kudhibiti vurugu hizo, gari la Polisi limepinduka wakati likiwa katika mwendo mkali kuelekea Mtwara na kujeruhi baadhi ya askari.
Baadhi ya Ofisi zilizochomwa moto ni pamoja na Jengo la Ofisi ya CCM saba saba, Hotel Shengena, ambayo imeelezwa kuwa ni moja ya Hoteli waliyofikia Askari wa Jeshi la Polisi (FFU) kutoka mikoa ya jirani kwa ajili ya kuongeza nguvu ya Operation ya vurugu hizo zinazoendelea.
Pia Nyumba kadhaa  za watumishi  wa Serikali  zimechomwa  moto maeneo ya Shangani, huku wananchi hao wakirundika Mawe na Magogo makubwa katikati ya Barabara ili kuzuia magari ya askari kufanya kazi ya kutuliza vurugu hizo.
Kufuatia vurugu hizo katika hali isiyokuwa ya kawadida, Spika wa Bunge Anne Makinda leo ameahirisha Kikao cha Bunge ili kutoa nafasi kwa Uongozi wa Bunge kukutana na kujadili kwa kina vurugu hizo za Mtwara na kutafakari ili kupata suluhu ya vurugu hizo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni